Tuesday, October 4, 2016

DC AHIMIZA UBUNIFU KWA WATUMISHI WA UMMA



Na: Stella Mmbando -  HAI

Mkuu wa Wilaya ya Hai  Gelasius Byakanwa amewataka wakuu wa idara na watumishi wote wa Wilaya hiyo  kujituma na kuwa wabunifu katika kutekeleza majukumu yao idara zao ili kuongeza ufanisi na kuimarisha ari ya kufanya kazi kwa maendeleo ya taifa.

Byakanwa alizungumza hayo wakati wa kutoa tuzo za mshindi wa shindano la ubunifu kwa idara na vitengo vya halmashauri hiyo ambapo mwezi huu zimeshindanishwa idara tatu ikiwamo idara ya mapato, biashara na mazingira.


Idara ya biashara ndio iliibuka na ushindi kwa mwezi Septemba ikizibwaga idara za mapato na mazingira ambapo washindi wameonesha ubunifu wa hali ya juu katika kukusanya mapato ya leseni kupitia viongozi wa vijiji na kuwa wameshakusanya mapato ya  zaidi ya shilingi milioni arobaini kwa kipindi cha miezi mitatu ikiwa ni sawa na asilimia hamsini ya lengo la idara kwa mwaka ambalo ni  shilingi milioni themanini na mbili laki moja na tisini elfu  huku wakibainisha kuwa bado zipo kata ambazo bado hazijafikiwa na uhamasishaji huo.

Imeelezwa mbele ya Mkuu wa Wilaya na majaji wa shindano na watumishi wote wa halmashauri hiyo kuwa wafanyabiashara mia nane walijitokeza kukata leseni za biashara ikiwa ni muitikio wa kampeni kabambe iliyofanywa na washindi kupitia matangazo na kutoa elimu kwa kutumia rediio inayomilikiwa na halmashauri.

Aidha kwa upande wao idara ya mazingira wameonesha ubunifu kwa kukusanya pesa katika kituo cha kutupia taka cha Tumaini, kuzalisha mbolea kutokana na taka pamoja na kukusanya na kuondoa taka katika barabara zote  zilizopo wilaya ya Hai.

Shindano la ubunifu maarufu kama “Byakanwa Awards” limeanzishwa na Mkuu wa Wilaya ya Hai Gelasius Byakanwa kwa lengo la kuinua ari ya utendaji miongoni mwa watumishi wa umma katika wilaya hiyo ambapo kila Ijumaa ya mwisho wa mwezi idara tatu zinawasilisha mbele ya majaji taarifa ya utekelezaji wa majukumu ikionesha ubunifu uliotumika na mafanikio yaliyopatikana huku wakitaja changamoto walizokutana nazo na namna walivyozipatia ufumbuzi.

No comments:

Post a Comment