Friday, May 18, 2018

Korosho kuimarisha Uchumi Wilaya ya Hai

Katibu Tawala Wilaya ya HAi Upendo Wella (aliyevaa miwani na skafu nyeusi) akiwaongoza viongozi wa ngazi mbalimbali kulipokea zao la korosho na kuinua juu miche ya zao hilo kama ishara ya kuinua uchumi katika Wilaya ya Hai (Picha zote na Praygod Munisi)

Na. Adrian Lyapembile
HAI

Wananchi wa wilaya ya Hai mkoani Kilimanjaro wametakiwa kuchangamkia fursa za kiuchumi kwa kushiriki kwenye kilimo cha mazao ya biashara likiwemo zao la korosho ambalo linastahimili hali ukame na kustawi kwenye mazingira ya ukanda wa tambarare wa Wilaya hiyo.

Zao hilo ambalo limetambulishwa kwa mara ya kwanza wilayani hapo kwa uzinduzi uliofanyika tarehe 17/05/2018 kwenye jengo la Kituo cha Rasilimali za Kilimo (WARC) lililopo kata ya Masama Rundugai.

Akizungumza kwenye uzinduzi wa zao hilo; Katibu Tawala Wilaya ya Hai Upendo Wella amewataka wananchi kujitokeza kwa wingi kuchukua miche inayogawiwa bure na serikali lakini pia kutoa maeneo yao kwa ajili ya kuotesha miche ya korosho kwani zao hilo ni moja ya mazao ya biashara yanayofanya vizuri kibiashara na litasaidia sana katika kuinua uchumi wa wananchi hasa wa ukanda wa tambarare.
“Natoa wito wa serikali kwa wananchi wa maeneo yatakayolimwa zao hili wakiongozwa na wenyeviti wa vijiji na viongozi wengine katika maeneo yao wahamasishane kuendelea kutenga maeneo ya kuotesha miche ya korosho ili kufikia lengo la kuotesha miche 5000 kwenye kila kijiji ili kuweza kuona tija na faida za zao hili” Amesema Wella.

Katibu Tawala Wilaya ya Hai Upendo Wella akipanda mche wa korosho kuashiria uzinduzi wa zao hilo mara baada ya kulitambulisha rasmi kwa wakazi wa Wilaya ya Hai.

Wella amewata wale watakaopatiwa miche inayogawiwa na serikali kuitunza vizuri kwenye mashamba watakapoipanda kwani serikali imetumia fedha katika kuandaa miche hiyo ili iweze kumfikia mwananchi bila gharama huku akiwaagiza wataalamu wa kilimo kuwafikia wananchi kwa ajili ya kuwapatia elimu na usaidizi wa kitaalamu wakati wa kutunza miti ya korosho kwa ajili ya kupata mavuno makubwa zaidi.
Akitoa salamu za wilaya kwa mgeni rasmi; Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Wilaya ya Hai Yohana Sintoo amewapongeza wananchi wa kata ya Masama Rundugai kwa namna wanavyolitunza na kulitumia jengo la Rasilimali za Kilimo kwa ajili ya kupata elimu ya mambo yanayohusu kilimo.
Aidha Sintoo amewahimiza wananchi kuona umuhimu wa kulima zao la korosho ambalo halina gharama kubwa katika matunzo lakini pia ni zao la muhimu katika uchumi wa viwanda litakalobadilisha hali ya kiuchumi ya wananchi watakaolima zao hilo.

Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Wilaya ya Hai Yohana Sintoo akiotesha mche wa korosho wakati wa uzinduzi wa zao hilo katika kuunga mkono juhudi za serikali kuhuisha kilimo cha mazao makuu matano ya biashara.

“Leo tunazindua rasmi kilimo cha korosho kwenye ukanda wa tambarare wa wilaya yetu; tuna furaha sana tumepata miche elfu 16 kutoka Bodi ya Korosho na tumeona vema kwanza tufanye shamba darasa kwenye eneo la heka 2 za Shule ya Msingi Rundugai litakalotumiwa na wataalamu wa kilimo kuwafundishia wakulima” ameongeza Sintoo.
Kwa upande wake Diwani wa Kata ya Masama Rundugai, Elibariki Mbise amewataka wananchi kupokea vizuri zao la korosho kwenye maeneo ya ukanda wa tambarare kwani ni sehemu ya kutunza mazingira lakini pia mavuno yatokanayo na zao hilo yatasaidia kuboresha uchumi wa wakulima huku akihusisha kwa karibu zao hilo na maendeleo ya viwanda.

Diwani wa Kata ya Masama Rundugai Elibariki Mbise akipanda mche wa korosho baada ya uzinduzi wa kilimo cha zao hilo linalotarajiwa kuwainua kiuchumi wananchi wa ukanda wa tambarare katika Wilaya ya Hai.

“Zao hili lina manufaa makubwa mbali na kuwa ni zao kwa ajili ya biashara lakini pia ni sehemu ya kuhifadhi na kutunza mazingira kama mti lakini pia tumeona umuhimu wa zao hili kwa uchumi kwani bei ya kahawa na bei ya korosho zinakaribiana. Sasa ukanda wa juu kahawa na ukanda wa tambarare ni korosho” Amesisitiza Diwani Mbise.
Naye Afisa Kilimo wilaya ya Hai, David Lekei amebainisha sababu ya zao la korosho kulimwa ukanda wa tambarare kuwa ni kwa sababu ukanda wa tambarare unapata mvua kidogo na kukaa muda mrefu katika hali ya ukame kitu ambacho zao la korosho linahimili.

Afisa Kilimo Wilaya ya Hai David Lekei akipanda mche wa korosho katika uzinduzi wa kilimo cha zao hilo katika shamba la Shule ya Msingi Rundugai.

Lekei ameongeza kuwa hadi sasa yamepatikana maeneo ya kuotesha miche ya korosho kwenye vijiji 23 vya kata tisa kukiwa na jumla ya hekari 643 zilizo tayari kwa ajili ya kuotesha miche huku wakulima 450 wameshajitokeza kutaka kuotesha miche ya zao hilo.
Kwa upande wao wananchi wa kijiji cha Rundugai walioshiriki kwenye uzinduzi huo wamesema wanafurahi kuona zao hilo limefika kwenye maeneo yao na wanategemea watafaidika na mavuno ya zao hilo katika kuboresha hali yao ya kiuchumi.

Bi. Mwanaisha Msuya akizungumza na waandishi wa habari kuelezea furaha yake baada ya kutambulishwa kwa zao la korosho katika Wilaya ya Hai.

“Kwa jinsi tunavyosikia wenzetu wa Mtwara na Lindi wanavyopata mazao mengi inatupa moyo na sisi kuwa tutapata mazao kwa ajili ya biashara ila tunaomba serikali iendelee kutuelimisha kuhudumia zao hili kitaalamu” amesema Mwanaisha Msuya mkazi wa Rudugai.
Uzinduzi wa kilimo cha korosho katika ukanda wa tambarare wa wilaya ya Hai mkoani Kilimanjaro umefanikiwa baada ya kukamilika kwa utafiti uliofanywa na wataalamu na kuthibitisha kuwa maeneo hayo yanafaa kwa kilimo cha zao hili huku ikiwa ni utekelezaji wa mikakati ya serikali ya kufufua mazao makuu matano ya kibiashara ya Pamba, Chai, Tumbaku, Kahawa na Korosho hivyo kufanya Wilaya ya Hai kupata mzao makuu mawili ya Kahawa kwenye ukanda wa juu na korosho kwenye ukanda wa tambarare.

Baadhi ya wanafunzi wa Shule ya Msingi Rundugai wakishiriki uzinduzi wa zao la korosho 



No comments:

Post a Comment